Facebook

PESA ZA SHEMEJI SEHEMU YA NANE 08

 


    Simu ya Inspekta Nyawenga ilimchanganya sana Esther na kumfanya asitishe jambo lile alilokuwa akilifuatilia. Ikabidi arudi katika eneo alilokuwa ameketi mwanzo pamoja na yule mfanyazi mwenzake. Wakati huo naye Dr. Adamu alikuwa akitoka nje ya ofisi ya Dr. Justine ambaye ndiye Daktari mkuu wa AGA KHANI Hospital.

Alielekea moja kwa moja upande alipokuwa amekaa Esther pamoja na mwenzake. Esther alipomuona Dr. Adamu alisimama na kumnyookea huku kila mmoja akimtizama mwenzake lakini macho na uso wa Esther uliokuwa umekunja ndita uliashiria moja kwa moja yakuwa alikuwa ni mtu mwenye hasira na aliyepaniki kwa wakati huo. “Vipi Mbona kama hauko sawa aliuliza Dr. Adamu “Ndiyo.. yeap yeap kuna… kuna jambo” alijibu Esther “Kwani utakuwa na ubaya kwa mimi kufahamu jambo hilo”  aliendelea kuhoji Dr. Adamu “Usijali Dokta waeza endelea na majukumu yako” Esther alijibu kama vile mtu aliyekuwa ahitaji ushirikiano kutoka kwa Dr. Adamu lakini hilo halikuweza kumsumbua wala kumkatisha tamaa Dr.Adamu ambaye alikuwa na mpango wa kuanza kuseti tageti zake kwa Esther.

Kulikuwa na kimya kidogo lakini haikuzidi dakika moja simu ya Esther ikaanza kuita alipotaka kupokea akashtuka kuona kwamba ilikuwa ni ile namba aliyotumia inspekta Nyawenga kumpigia kwa  mara ya kwanza na kumtaka afike eneo la tukio la ajali ya Boss France. Alisita kidogo nayo simu iliendelea kuita akaona hakuna namna nyingine zaidi ya kupokea simu ile. “Haroo... Vipi umeshaanza kuja tunakusubiri tuanze majukumu yetu” alisema inspekta nyawenga kwa ukali kidogo “Abee… nakuja  Afande”  aliitikia Esther aliyekuwa akionyesha hali ya uoga kiasi kwamba Dr. Adamu alishindwa kuelewa ni kipi kulichokuwa kinamsibu Esther. Basi Esther alibeba pochi yake na kutoa kiasi cha noti nyekundu kisha akampatia yule mfanyakazi aliyekuwa amekuja naye pale hospital na kumtaka aendelee kubaki kwa ajili ya kumpa taarifa zitakazoendelea juu ya Boss wake.

Alimpungia mkono Dr. Adamu na kuanza kuondoka lakini ghafla alijikuta akizuiliwa na kuvutwa na mkono wa Dr. Adamu Kisha akajiwahi Aaah! Samahani Esther kwa kukuzuia lakini nafikiri ni vema ukanipa namba yako ili tuweze kuwasiliana juu ya hali ya mgonjwa wako” “utampatia taarifa huyu mfanyakazi alafu atanijuza mimi” looh…! Mwanadada Esther alikuwa na majibu yaliyomchoma sana moyo Dr. Adamu na kumfanya ashindwe kuelewa ni wapi alipokosea.

Wakati hayo yote yalipokuwa yakiendelea naye Dr. Justine aliweza kuyashuhudia kwani alikuwa akitoka nje ya ofisi yake lakini baada ya kuona mwanzo wa jambo lile alisimama kwa mda nje ya mlango wa ofisi yake na kulitolea macho. Alitingisha kichwa na kucheka kidogo kwa tabasamu kisha akaondoka kuelekea katika wodi aliyokuwa amelazwa Vicky. Wakati huo Esther alikuwa akielekea sehemu alikopaki gari huku akitembea kwa mwendo ya madaha,  mavazi ya Esther aliyokuwa ameyavaa siku hiyo ukichanganyia na uzuri wake uliochagizwa na rangi yake ya mvuto na iliyo asilia ilimfanya Dr. Adamu kuingia mzima, mzima kwa Esther kifikra bila hata ya kugonga hodi. Loooh! Alichanganyikiwa bila ya kujua ni wapi alipokuwa akipakimbilia. Esther aliingia ndani ya gari lake na kuanza kuondoka kuelekea katika eneo la tukio la ajali ya Boss France. Kichwa chake kilikuwa resi na kikiwaza juu ya hali aliyokuwa nayo Boss wake na huko aendako “Sijui kuna nini cha zaidi na sijui ni kipi hasa ninachoenda kukijibu  huko” alijihoji Esther katika fikra zake wakati  alipokuwa njiani  kuelekea sehemu ya tukio la ajali.

Aliyakanyaga mafuta ya gari na kumfanya atumie mda mchache kuwasili eneo hilo. Kabla hajashuka kutoka kwenye gari lake aliliona jopo la maaskari kadhaa waliokuwa wamevalia reflekta nyekundu. Alishuka na kuelekea katika kundi lile na askari na kabla hajasema chochote alisikia sauti ile ya inspekta Nyawenga ikimkaribisha  Habari! Bila shaka wewe ndiye sekretari Esther”Ndiyo haujakosea afande” alidakika Esther kwa haraka haraka. “Sisi ni timu ya askari wapelelezi na usalama hivyo tumefika hapa kwa ajili ya kuchunguza ajali iliyotokea hapa na kuchukua taarifa zake, kikubwa  tunaomba ushirikiano katika hili” alizungumza inspekta nyawenga naye Esther hakusita kuwapatia ushirikiano juu ya tukio lile.

Mmoja wa askari aliyekuwa ameshikilia kijitabu kidogo cha kuchukulia maelezo pamoja na kalamu alianza kumhoji Esther aliyekuwa akijibu kwa sauti ya mapozi. Zoezi lile lililopaswa kuchukua dakika kumi na tano ilibidi ligharimu muda wa nusu saa kwani sauti ya mapozi iliyokuwa ikitoka kwenye kinywa cha Esther pamoja na mavazi yake aliyokuwa amevalia siku hiyo yalianza kumhamisha kamanda aliyekuwa akihoji juu ya suala zima la ajali na kujikuta akihoji juu ya masuala mengine yasiyohusika. Kamanda huyo alimalizia mahojiano hayo kwa kumuuliza Esther kama ameolewa au lah! … kwa ufupi kamanda naye alianza kujikuta akiingia katika mtego wa Esther bila ya kujielewa.  Muda kidogo baada ya mahojiano inspekta nyawenga alitoa shukrani zake kwa Esther juu ya ushirikiano aliouonyesha katika zoezi lile bila ya kutambua yakuwa askari aliyehusika kufanya kazi hiyo alikuwa ameshaanza kumtamani Sekretari Esther.

Inspekta nyawenga pamoja na  na jopo lake walimuaga Esther na kisha wakaondoka kuelekea kutimiza majukumu yao. Naye Esther alielekea moja kwa moja ndani ya HYATT REGENCE HOTEL. Kila mfanyakazi ikiyemuona siku hiyo alikuwa na shauku ya kutaka kufahamu juu ya hali ya Boss France,  na kutokana na haraka aliyokuwa nayo ya kutaka kurudi hospital kwa ajili ya kuhakikisha uangalizi wa karibu wa Boss wake ilimuiwa vigumu kuzungumza na kila mfanyakazi. Alitembea haraka haraka kuelekea katika ofisi yake na kuandika taarifa juu ya hali ya Boss France pamoja na kuahirisha kikao kilichopaswa kufanyika siku hiyo “Hali ya Boss wetu siyo mbaya na madaktari wanaendelea kupambana ili kuhakikisha anakuwa salama na pia kikao kilichopaswa kufanyika siku ya leo kimehairishwa mpaka pale kitakapoitishwa tena, Ahsanteni!” la hasha! Ulikuwa ni ujumbe ambao ungewafanya wafanyakazi washindwe kufanya kazi zao kwa ufanisi ndani ya siku kadhaa.

Baada ya kuandika ujumbe huo alinyoosha mkono  mpaka kwenye pochi yake akaibeba na kuelekea upande wa sehemu iliyokuwa na kioo cha kujiweka sawa. Alijitazama kwa muda kidogo kupitia kioo kile na kubaini ya kuwa hata macho yake yanayoonekanaga kuwa na mvuto wa aina yake yalimsaliti kwa siku hiyo kwani sura ya kupooza na uso wenye wimbi la huzuni vilimgubika. Hatukata kupoteza muda alijifanyia make up ya dakika chache kisha akabeba pochi na simu yake,  alipotaka kutoka nje ya ofisi yake akakumbuka yakuwa aliuacha ujumbe wa taarifa juu ya hali ya Boss France. Alirudi akauchukua kisha akaupeleka moja kwa moja katika moja ya ofisi za kusambaza taarifa. Baada ya kufanya hivyo Esther alitembea kuelekea nje ya jengo hata hivyo ilikuwa ni ngumu kwa baadhi ya wafanyakazi wenzake waliomuona kuweza kumsemesha kwani hata uso wake ulikuwa ukisema wenyewe yakwamba hakuwa katika hali nzuri.

Wakati huo ndani ya AGA KHANI Hospital ulikuwa ni wakati maalumu kwa ajili ya kuonana na wagonjwa naye mfanyakazi aliyekuwa ameachwa na Esther pale Hospital kwa ajili ya kumpatia taarifa juu ya hali ya Boss France alielekea katika ofisi ya Dr. Justine na kabla ya kubisha hodi aliitwa na Dr. Adamu aliyehitaji kumuuliza jambo. Ilikuwa ni muda wa saa nane kasoro mchana ambapo hata naye Dr. Adamu alipaswa awe amekwisha kuelekea nyumbani kwake kwa ajili ya mapumziko. “Samahani dada,  kuna jambo nahisi kama vile halijakaa sawa kwa Esther kwani nini kilimsibu tofauti na hili la Boss wake kupata ajali” aliuliza Dr.Adamu Kiukweli mimi mwenyewe sifahamu chochote kinachoendelea” alijibu mfanyakazi yule huku nafsi yake ikimsuta dhairi yakuwa alikuwa akizungumza uongo lakini kama ilivyokuwa ada kwa Dr.Adamu naye hakusita kuendelea kuhoji. “Kwani wewe unahisi kuna nini?, Ama kuna tatizo kazini kwake? na pia unaitwa nani?” Looh! Yalikuwa ni maswali magumu kwa mfanyakazi huyo kuweza kuyajibia yote kwa wakati huo kwani Dr.Adamu aliuliza maswali matatu kwa mfululizo. “Naitwa Grace” Dr. Adamu akadakia kwa mkazo Gracee“Ndiyo Grace na ndilo jina langu kuhusu mengine sifahamu chochote”  Grace alimjibu Dr. Adamu kana kwamba alikuwa ni mtu aliyepandikiziwa kiburi na Esther.

Naye Dr. Adamu aliweka mkazo juu ya jina la Grace kwa vile jina hilo halikuwa ni geni kwake kwani lilikuwa ni jina sawa nala mpenzi wake walieachana wiki chache zilizopita. Grace alitaka kugonga hodi katika ofisi ya Dr. Justine lakini Dr. Adamu alimtaka kuendelea kusubiri kwanza ili akamilishe adhma yake. Dr. Adamu aligeuka na kukielekeza kichwa chake juu kisha akaanza kugongagonga kwa kukikutanisha  kidole chake cha Gumba na cha Ada dizaini ya mtu alikuwa akifikiri kutaka kupongeza juu ya jambo fulani. Aligekuka tena na kumtizama Grace ambaye naye alikuwa akimtizama Dr. Adamu kwa umakini mkubwa,  “Ahaaaaaah…! Alafu nafikiri huu ni muda sahihi kwa ajili ya kuwaona wagonjwa sindivyo” alihoji Dr. Adamu huku akimtolea macho Grace aliyeanza kumjibu “Mimi sijui ndo mara yangu ya kwanza kuwepo hapa” Dr. Adamu alijaribu kutumia mbinu mbalimbali za kumfanya Grace aweke umakini mkubwa kwake lakini ilikuwa ni sawasawa na bure kwani kila mbinu iligonga mwamba huku lengo lake hasa ni kutaka kupatiwa namba na Esther.

Basi hakuwa na namna zaidi ya kuwa muwazi kwani alimuomba Grace ampatie namba za Esther naye Grace alikuwa mbishi,  akajaribu kumuomba kwa mara nyingine lakini ikawa ni jambo gumu tena. Na hapo ilimbidi apeleke mkono wake katika mfuko wa nyuma wa suruali yake na kutoa kiasi cha pesa kilichokuwa kimesheheni noti nyekundu kisha akamnyooshea Grace Loooh! Pesa ni pesa tu. Kwani Grace akusita kuachia tabasamu zito na kuanza kuitafuta namba ya Esther katika simu yake bila ya kuambiwa chochote kile na Dr. Adamu. Grace alimtajia  Dr. Adamu namba za Esther na zakwake pia na kisha wakaangaliana kwa muda na wote wakatabasamu.

Wakati huo akili ya Grace ilisahau hata juu ya kile alichokuwa akitaka kukifanya, akajikuta akielekea Restaurant kwa ajili ya kupata chakula naye Dr. Adamu alielekea katika ofisi yake . muda huo alionekana kuwa mwingi wa tabasamua na furaha ilifikia hatua akawa anajitazama kwenye kioo cha simu yake na kujicheka juu ya kile alichokuwa akikifanya. Hakutaka kupoteza muda na mara moja alitaka kuipigia namba ile lakini alikuwa na dalili za uoga,  uoga. Alijikaza kisabuni na kisha akaipigia namba ya Esther nayo simu ikaanza kuita na haikuchukua sekunde kadhaa simu ile ikapokelewa. “Hallo.. hallo..” “Yes  Hello!” aliitikia Esther kisha akauliza “nani mwenzangu?” “A’m a’m Dr. Justine.. Justine… hapa sijui umenisikia.. uko wapi” aliongea kwa utata mwingi kiasi kwamba hata naye Esther alishtukia jambo lakini hakusita kumwambia kwamba yupo njiani amekaribia kufika Hospital.

Baada ya kukata Simu Esther alijaribu kupiga namba ya Dr. Justine aliyoichukua kwenye chumba cha mapokezi pale hospital na namba hiyo ilikuwa hewani lakini iliita tu kwa muda bila ya majibu. Kumbe wakati huo Dr. Justine alikuwa ametoka kidogo katika ofisi yake na kuacha simu ndani,  naye Dr. Adamu moyo wake ulianza kumwenda mbio na kujijutia juu ya uongo aliojikuta ameuzungumza bila ya kujielewa. Laah.. hasha!! Mawazo yake yalitofautiana na akili yake. Alibaki kuwa mtu wa kuchungulia upande wa chini kupitia kwenye dirisha lake na ghafla.. alibahatika kuliona gari la Esther lililoingia kwa kasi kwenye geti la Hospital Hoooh! Alijitolea macho kwa hofu na mashaka na hapo hakuwa tayari kusubiri timbwili na mwanadada Esther kwani alitoka haraka haraka ndani ya ofisi yake na kukumbilia upande wa mlango wa pili kuelekea Restaurant.

Mwisho

Je,  ni nini kitakachoendelea baada ya Esther kwenda kujua ukweli juu ya simu ya Dr. Adamu aliyedanganya yakuwa yeye ni Dr.Justine?

Usikose mwendelezo wa sehemu ya tisa 09


Mwandishi: Sebastiani Masaba 

Phone: 0746445197


Post a Comment

0 Comments