Facebook

SUKARI YA KIJIJI SEHEMU YA PILI 02

 


Hatimaye ikawa ni moja ya siku mbaya na isiyobahati kwa Mijanja na hata kwa familia ya Mzee Magoti kwa ujumla wao kwani kila mmoja alipopata taarifa hizi alibaki akiduwaa na kustaajabu kwa yaliyotokea na mbaya zaidi Msichana yule alitoweka usiku kwa usiku katika mazingira ya kutatanisha pasipo wao kuweza kumfahamu hata kwa jina.

Baada ya usiku huo wa kizaazaa kupita   Mzee Magoti aliamua kukaa pamoja wa familia yake ili kuweza kujadili kidogo juu ya lile tukio kwani lisingeweza kuwa la kawaida hasa kwa mtu aliyeweza kusaidiwa na kupewa hifadhi kisha akatoweka hata kabla ya mawio kuwia. Mzee Magoti alihoji huenda binti yule alikuwa ni kiumbe kisicho cha kawaida Mzee Magoti: “Isije ikawa tulitoa msaada na kukaribisha jini ndani ya nyumba yangu” . Lakini hakukuwa na hata mmoja wa wanafamilia wake aliyeweza kutoa jawabu juu ya tukio hilo huku hofu na uoga ukiwatanda katika fahamu zao.

Jambo lile likaendelea kubaki kuwa la siri ndani ya familia ya mzee magoti bila hata ya mmoja ya wanakijiji wengine kuweza kufahamu. Mijanjaa alirejea ndani ya chumba chake na kujitupa kitandani mwake alikuwa mwenye sononeko la moyo na aliyekosa amani akajiuliza ndani ya nafsi yake “ “Hivi kweli inawezekanaje mtu kuweza kufanya jambo hili la kutoweka tena ikiwa ni mtoto wa kike,  na giza lote lile, mvua yote na radi yate ile iliyokuwa ikinitisha hata mimi hapana kwakweli bado hainiingii akilini” Aliendelea kuwaza na baada ya sekunde chache akakumbuka juu ya rafiki yake mkubwa aitwaje Mwagani.

Huyo alikuwa ni rafiki mkubwa wa mijanja na ambaye amekuwa akimshirikisha mara nyingi juu ya mambo yake hata wakati wa kuwinda pamoja na kuteka maji mtoni hupenda kuwa pamoja naye. Hatimaye siku hiyo mada kuu iliyotawala katika vijiwe mbalimbali ndani ya kijiji cha korona ilikuwa ni kuhusiana na radi kubwa na hali ya ajabu ambayo haijawahi kutokea katika kijiji hicho kwa miaka mingi.

Zuena mama wa familia na mke wa Mzee magoti alikuwa akifagia,fagia katika eneo la nyumba yake, na mara tu alipogeuka na kuangusha macho yake mbele  alibahatika kuona cheni yenye rangi ya dhahabu iliyokuwa imetepeta kwa damu nzito lakini kila alipojaribu kuisogelea kwa ukaribu zaidi,  aliona ile rangi na kile kiwango cha damu kikizidi kutoweka katika cheni ile. “Kheeeh! Hichi ni nini tena? mbona sijapata wahi kuona katika maisha yangu yote” alijuuliza Zuena huku akipigwa na butwaa na asijue afanye nini kwa wakati huo lakini wakati akiendelea kuduwaa na fahamu zake kudhoofu kutokana na tukio lile kwa mbali alisikia mluzi ukipigwa,  mluzi huo ulipigwa mara tatu ikiwa ni alama ya kuashiria jambo fulani.

“Hodi hodi hodi” “karibu” hiyo ilikuwa ni sauti ya Mwigani rafiki yake na Minjaa iliwepewa heshima ya kakaribishwa na Zuena.    

Mwigani: Shikamoo Mama

Zuena: Marhaba mwanangu karibu

Mwigani: Ahsante mama,  Nimekuona tokea mbali ukiwa unaangaza chini kwa muda mrefu sana tena kwa mshangao mkubwa Je,  kuna nini?

Zuena: hakuna lolote mwanangu hata usijali,  rafiki yako yuko ndani unaweza ukamuona. Majibu ya Zuena yalimfanya Mwigani achezwe na chale na kuhisi huenda kuna jambo alililofichwa na Zuena hivyo akaamua kupitiliza moja kwa moja hadi kwenye chumba cha mijanja na kumkuta rafiki yake akiwa katika hali ambayo hakuwahi kuizoea. Siku hiyo Mijanja hakutaka rafiki yake Mwigani  aweze kubaini jambo lolote juu ya lile lililoikumba familia yake. Alijichangamsha na kujifanya mwenye furaha kila wakati ilihali tu kumfanya rafiki yake asiweze kugundua jambo lolote. Muda ulikwenda mpaka kufikia majira ya saa kumi na mbili jioni huku wawili hao wakiwa katika wimbi la stori mbalimbali zilizohusiana na kijiji chao. Mwigani alifikiri kidogo na kumtaka rafiki yake Mijanja walau waweze kutoka nje kwa mda kwani walikaa ndani kwa muda mrefu mpaka kufikia majira ya jioni. Mijanja alifikiri juu ya wazo la rafiki yake huku vidole vyake vikiendelea kuburudisha udevu wake kwa kuukunakuna. Baada ya sekunde chache aliapata wazo alilolihisi huenda lingefaa zaidi “nafikiri ni kheri tukatweke maji mtoni” alisema mijanja huku akiendelea kumchagiza rafiki yake mwigani kwamba huko wangeweza kupata upepo mzuri na tulivu pamoja na sauti nzuri na zenye kuvutia za ndege wa aina mbalimbali. Mwigani hakuwa na shaka wala ubishi wowote juu ya wazo la rafiri yake hivyo walibeba mitungi ya maji na kuelekea katika mto yambwa.  

Wakati huo ilikuwa ni jioni tulivu ambayo haikuwa na purukushani za watu wengi kuelekea wala kutoka mtoni. Upepo tulivu na wenye kiubaridi chenye ushawishi nayo ulikuwa ukiyanong'oneza masikio yao, sauti za kuvutia za ndege mbalimbali na zilizokuwa na uwezo wa kuyashibisha masikio yao nazo zilikuwa zikivuma kwa ustadi wa aina yake,

Maua mazuri ya kupendeza pale uyatazamapo na yenye rangi mbalimbali zenye uwezo wa kuyalisha macho na kuyafanya yaweze kushiba nayo yalishamiri pembezoni mwa njia iliyokuwa ikielekea mtoni. Mijanja alisogea pembeni na kuchuma moja ya ua lililokuwa limemvutia kisha akalinusa. Ua lile lilikuwa na harufu nzuri sana lakini kitendo kile kiliweza kupelekea mwili mzima wa mijanja kusisimka kama mtu aliyepigwa na shoti lakini hakujali kuhusu hilo kwani alilitupa ua lile na kuendelea na safari yao.

 Walitembea kwa muda kidogo na wakawa wamekaribia kufika katika mto yambwa. Kwa mbali kidogo Mijanja aliona Kama kuna mtu mmoja aliyekuwa akiogoa pale mtoni, alimgusa rafiki yake begani na kunyoosha kidole chake kimoja kule mtoni ikiwa ni ishara ya kumjuza juu ya jambo lile. Mwigani alishtuka na kujiziba mdomo wake ili asiweze kupiga kelele kwani alipomtazama vizuri mtu yuke aligundua ya kuwa alikuwa ni msichana. Mwigani alishtuka zaidi maana pia kwake lilikuwa ni jambo geni kulishuhudia. Walisogea pembezoni mwa mti mrefu na kujibanza ili kuendelea kumtizama yule msichana.

Hawakuweza kumuona msichana yule vizuri kwa kadri ya matamanio ya hisi zao ikabidi wapende juu ya ule mti ili waweze kuyafurahisha macho yao zaidi. Walipofika juu ya mti ule kila mmoja aliweza kumuona na kumtizama msichana yule vizuri zaidi. Laaah! Mash allah!... Hakuna hata mmoja aliyeweza kutaraji wala kuwahi kufikiri kumuona msichana wa dizaini ile katika maisha yao pale kijijini Kwani alikuwa ni msichana aliyejikamilisha kwa kila kitu kuanzia juu mpaka chini.

Msichana huyo alionekana kuwa na rangi nyeupe katika mwili wake, kichwa chake kilifunikwa na nywele ndefu za singasinga zilizokolea weusi mtupu na zilizokuwa zimetanda katika mgongo wake, Miguu ya bia balimi iliyokuwa imeungana na paja zenye chirizi za mbali, shepu lake matata lilijichora umbo namba nane isiyokuwa katikati ya sita wala saba, huku Kilimanjaro mlima ukimea pale zilipoishia nywele zake. Loooh....!!! Kwa ufupi alikuwa ni msichana mzuri sana ambaye angeweza kuzikonga hata nyoyo za wavuvi kulima mpunga pale akatizapo mbele ya macho yao. “Mhhhh...! Kwakweli sijapataona jambo kama hili tangu nimezaliwa” Alitoa ghuno Mwigani ambaye pia aliendelea kuwa na kiwewe cha kustaajabu juu ya jambo lile.

Mijanja alitamani ashuke juu ya mti na kumfuata msichana yule pale mtoni lakini rafiki yake alimzuia kwani bado alikuwa na moyo wa shaka kwani haikuwa ni jambo la kawaida kumuona msichana mzuri kama yule akiwa pale mtoni peke yake kwa muda kama ule. Lakini ilikuwa ni ngumu kwa mijanja kuweza kuelewa akisemacho rafiki yake kwani akili na fahamu zake zilishapaa juu zaidi. “Hapana Mwigani nadhani ni msichana wa kawaida kama walivyokuwa wasichana wengine hapa kijijini ila tu kawazidi kwa uzuri” alisema Mijanja huku akiendelea kushuka kwenye mti kuelekea mtoni alipo yule msichana. Mwigani naye aliona kuna haja ya kushuka na kumfuata rafiki yake.

Mijanja alikuwa wa kwanza kuteremka na kuanza kujongea kumfuata yule msichana,  lakini kila alipoendelea kusogeza hatua zake mapigo ya moyo yalimwenda kasi na mwili ulizidi kumsisimka kwa ouga ambao hakuweza kutambua ulitoka wapi. Wakati huo giza jembamba lilianza kushamiri na punjepunje za baridi nazo ziliendelea kukolea pale mtoni.

Mijanja aliendelea kujongea na kufika karibu zaidi kwa yule msichana aliyekuwa amegeukia upande wa pili na kuucha wazi mwili wake wote kwa upende wa nyuma. “Muyara.. awee muyara...” aliita muyara akimaanisha msichana kwa lugha yao lakini msichana yule hakuweza kugeuka wala kusema chochote zaidi na kuendelea kuyachezea maji kwa mikono yake. Naye Mijanja hakukata tamaa bali aliendelea kuita huku akiwa na shauku ya kutaka kumtambua msichana yule pindi atakapogeuka.

Ghafla msichana yule aligeuka huku akitabasamu bila ya kusema chochote na ilikuwa ni baada ya mijanja kumuita mara tatu tatu mfululizo “Muyara, muyara,  muyara” loooh! Mijanja alijikuta akishtuka kwa uoga uliomuingia na kuteleza kuangukia ndani ya mto alipokuwa yule msichana.  Mwigani rafiki yake na Mijanja aliyekuwa na hofu tangu mwanzoni alipiga mbiu kwa nguvu iliyoweza kusikika kule kijijini kisha akaanza kukimbia baada ya kushuhudia tukio lile lililomkuta rafiki yake. Alikimbia kwa kasi huku mwili mzima ukimtetemeka na jasho zito likimmwagika mara ghafla alijikuta akikitwa na kitu kizito kisichofahamika kichwani mwake, akaanguka chini na kupoteza fahamu zake.

**MWISHO**

Endelea kufuatilia miendelezo ya tamthiliya hii ili uzidi kuburudika na kuelimika


Mtunzi na mwandishi- Sebastian masabha

Mobile no: 0758-162527

Whatsapp 0746-445197


Post a Comment

0 Comments