Facebook

PESA ZA SHEMEJI SEHEMU YA 11

Kile kibao kizito alichokipokea dkt. Justine kutoka kwa Esther ilikuwa ni ishara tosha ya kwamba hakuwa katika matazamio yoyote ya kihisia kwa Esther. Aliokota miwani yake na kuelekea katika gari lake huku akitoa maneno yenye vitisho kwa Esther ya kwamba ipo siku utakuja kunipigia magoti naye Esther aliyekuwa mwingi wa hasira na mawazo kwa wakati huo hakusita kumjibiza Dkt. Justine na kwa kumwambia “Nadhani pengine utaanza wewe na mimi ndo nitafuatia kufanya hivyo”  ikawa hivyo na hatimaye hakukuwa na namna ilibidi Esther kuwabeba akina Vicky na Boss France kwa pia kwa ujumla wao walikuwa wakikaa maeneo ya jirani ambapo Boss France aliishi Oysterbay, naye Esther pamoja na Vicky waliishi Masaki tofauti ilikuwa ni majengo tu. Kabla ya kuanza kuondoka Esther alimsihi Vicky aje akae eneo la mbele kwa pembeni yake na kumuacha Boss France akae peke yake kwenye siti ya nyuma ya gari. Boss France na Vicky walitizamana na kisha wote wawili wakatingisha vichwa vyao kuonesha kukubaliana na ombi la Esther ambaye kwa wakati huo alikuwa ameegemea na kuinamisha kichwa chake katika usukani wa gari. Basi zoezi hilo lilifanyika na kisha safari ya kuelekea majumbani ikaanza.

Ukimya ulitawala kwani hakukuwa na hata mmoja aliyeweza kumsemesha mwenzake ingawa kila mmoja alikuwa na dukuduku zito ndani ya moyo wake juu ya mwingine. Esther alijitahidi kuendesha gari kwa kasi ili wawahi kufika licha ya uwepo wa foleni kubwa iliyokuwa ikiwakabili njiani. Hatimaye waliingia mtaa wa Oyster bay naye Boss France kwa kuvunja ule ukimya uliokuwa umetawala mule ndani ya gari akasema “Thank you God niliumisi sana huu mtaa hasa nyumbani kwangu” alizungumza maneno hayo ikiwa ni ishara ya kwamba walikuwa wamekaribia kufika katika jumba lake.

Pia akajifanyisha kujinyoosha huku shingo yake na macho yake yakiwa mbele kumtizama Vicky ambaye alikuwa akitabasamu tu kwani alikwisha kuona vituko vyote vya Boss France kupitia kwenye kioo kulichokuwa mbele ya upande wa juu wa ndani ya gari. Esther alimtaka Boss France kumuelekeza njia iliyokuwa ikienda moja kwa moja hadi nyumbani kwake kwani alikuwa apafahamu mbali na kufahamu tu ya kwamba Boss wake alikuwa akiishi katika mtaa huo. Naye Boss France alifanya hivyo wakati hivyo wakati huo Esther na Vicky walikuwa wakiikodolea macho mijengo mbalimbali yenye hadhi ya aina yake iliyokuwa imepangika ndani ya mtaa huo. Ilichukua dakika mbili wakawa wamefika nje ya jumba la Boss France na kisha wote wakashuka na kuinua macho mbele yao.

Looh! Lilikuwa ni jumba hasa lenye ukubwa wa aina yake na muonekano mzuri uliowavutia na ambao ungeweza kumvutia yoyote yule kila alitazamapo. Boss France aliwakaribisha waingie ndani wakati huo geti la jumba lake lilikuwa likifunguliwa na Malila Mwanajogini baada ya Boss France kubonyeza switch iliyokuwa ukutani na kufanya mlio wa alamu isikike upande wa ndani wa jumba lake. “Karibuni sana, karibuni ndani na haka ndiko kajumba kangu” maneno haya yalitoka kinywani mwa Boss France huku akijichekesha. Mmh! Ilikuwa ni kauli ya kujikosha kwelikweli kwani kwa hadhi na heshima ya jumba lile hakupaswa kutoa maneno yale. Maneno yale yalikuwa si mali kitu kwa Esther na Vicky ambao hawakusita kuendelea kuonyesha namna ambavyo walikuwa wamekoshwa na muonekano wa mjengo ule. “Wow! ama kweli Boss wangu unaishi katika falme ya aina yake maana siyo kwa mjengo huu, Hongera zako” alizungumza Esther huku akiendelea kupepesa macho yake kushoto na kulia mwa jumba lile. Boss France alitabasamu na kuachia kicheko chepesi kisichokuwa na sauti kisha akasema asante. Vicky aliyekaa kimya kwa muda kidogo naye alidakia kwa maneno yake “Looh! Kwa mara ya kwanza naingia ndani ya mjengo wa Boss” Ewaah! Mapigo ya moyo wa Boss France yalipiga shwangwe kwani alifurahia jambo lile kimya kimya ndani ya moyo wake huku akili na hisi zake zikitoa majibu “Yes yajayo yanafurahisha” lakini haikuwa bahati kwa Boss France kwa wakati huo kwani hisi zile zilikatishwa na maneno ya Esther aliyedakia kwamba “Asante sana Boss Kwa ukaribisho wako nadhani tutakuwepo hapa kwa wakati mwingine, uzuri tushapafahamu wala usijali nitakuja sana acha kwa sasa tuwahi majumbani mwetu” kila mmoja alionyesha kucheka kidogo na kutabasamu ingawa kauli hiyo ya Esther yenye umimi iliacha maswali kadhaa katika kichwa na Boss France na Vicky. Lakini kabla ya moja kwisha la pili likajitokeza kwani Esther alimsogelea Boss France na kumpa kumbato zito lililokuwa joto la kimahaba ambalo ilikuwa ni vigumu kuweza kuzipima nyuzi joto zake hata kwa matumizi ya kipima joto. Baada ya hapo Esther alimshika Vicky kwa mkono mmoja huku mwingine akiubusu na kumpungia Boss France ikiwa ni ishara na kumuaga.

“Twende zetu shoga yangu muda umetutupa mkono” alikuwa ni Esther aliyeyasema hayo huku akielekea ndani ya gari lake. Wote walipanda na kuelekea Masaki yalipo makazi yao lakini Vicky alikuwa mwenye hasira na asiye na furaha kwa wakati huo juu ya kile kilichofanywa na Esther mbele ya macho yake alijisemea moyoni mwake “ama kweli leo umeniweza ila nitalipiza hili” ilikuwa ni tofauti sana kwa upande wa Esther kwani yeye alionekana kuwa na furaha kana kwamba kuhisi dunia ni yake ya peke yake na aliyempenda. Vicky alizidi kuchukia sana na kubaki na lake la moyoni juu ya Esther.

Ilichukua dakika kadhaa wakawa wamefika maeneo ya masaki lakini kutokana na hasira alizokuwa nazo Vicky hakutaka hata Esther afahamu alipokuwa akiishi. “Naomba nishushie hapo dukani kwa Mangi nadhani nitakuwa nimefika” alizungumza vicky huku Esther akimjibu “Noo... Vicky usijali nitakufikisha hadi nje ya jumba lako” maneno hayo yaliyokuwa ya kejeli kutoka kwa Esther yalizidi kumkwaza sana Vicky naye hakusita kujibu “Hapana nishushe hapo panatosha maana kuna vitu pia nahitaji kuchukua hapo dukani na kwangu siyo mbali na hapa Esther hakuwa na Budi kukubaliana na ombi la Vicky lakini kabla ya kufanya hivyo alimtaka Vicky aweze kumuazima masikio yake kwa dakika chache “ Vicky najua wewe ni mwanamke kama mimi na isitoshe ni mwanamke mzuri sana na mwenye mvuto kwa mwanaume yoyote yule ...” kabla ya Esther kutaka kumaliza alichokuwa amekikusudia ikiwa kama ni ujumbe kwa Vicky alikatishwa na sauti ya Vicky aliyezungumza kama vile mtu aliyekwisha kulitambua lengo la Esther “ Kwa hiyo Esther unataka kusema nini? Labda uzungumze kingine nitakuelewa lakini siyo kuhusiana na Boss France”  “Nashukuru kama utakuwa umeanza kulipata picha lake hivyo ninachomaanisha ni kwamba ukae mbali na Boss France” Esther alizungumza kwa kufoka lakini ilikuwa ni sawa na kazi bure kwani Vicky naye alimjibu kibabe “Kikubwa ni Boss wetu sote. upo mwanadada, hivyo kila mmoja acheze kwa muda wake alaaah! Kisha akashuka na kubamiza mlango wa gari kwa nguvu na kufyonza kwa sauti. Hakukuwa na namna kwani walishindwa kuelewana ikabidi Esther awashe gari na kuondoka kuelekea nyumbani kwake.

Vicky hakufurahishwa hata kidogo na kauli za Esther kwani aliitafsiri kama zilikuwa ni kauli za dharau na zenye kuwekeana masharti mahala pasipo hitajika kuwa na masharti. Vicky alikuwa mwenye uchovu wa aina yake kwa siku hiyo kwani pia alikuwa ametoka katika hali ya kuumwa ambapo alilazwa AGA KHAN hospital ndani ya siku kadhaa. Alitembea na kuelekea nyumbani kwake akiwa mwenye fungu zito la mawazo.

Upande wa Boss France ambaye aliachwa katika wimbi zito la hisi zilizoambatana na maswali kichwani mwake, alikuwa akitembea tembea kulia na kushoto mwa nyumba yake pamoja na Malila mwanajogini ambaye alikuwa na furaha kubwa ya kuona Boss wake amerejea nyumbani. Walipiga stori mbili tatu lakini kutokana na uchovu mwingi aliokuwa nao Boss France alionelea kwamba wangeendelea na mazungumzo yao kwa siku ya kesho kwani alikuwa akihisi usingizi.

Malila mwanajogini aliuliza kwamba naweza nikakuandalia chochote kitu Boss wangu naye akamjibu kwamba asijali kwani angeweza tu kuchukua juice kwenye friji na kuinywa. Aliingia ndani ya jumba lake na kuelekea katika moja ya friji yake ya kuhifadhia vinywaji na kuchukua juisi ya embe iliyokuwa katika pakti na kuingia ndani ya chumba chake kisha akayavua mavazi aliyokuwa nayo. Alifunga taulo lake kiunoni na kuelekea bafuni kujimwagia maji walau kuweza kupunguza kasi ya uchovu aliokuwa umeubeba mwilini mwake. Baada ya dakika chache alitoka bafuni na kurejea katika chumba chake kisha akabadili taulo kwa kuvaa mavazi ya kulalia. Alijiachilia na kujitupa kitandani mwake, kitendo ambacho kilimfanya anesenese mara kadhaa kulingana na namna ambayo kitanda chake kilivyokuwa kimetengenezwa. “Ahooooh! Ahaaah!...” alipiga mihayo huku akijinyoosha pale kitandani, punde kidogo aligeukia upande wa pili na kujilaza kifudifudi, alinyoosha mkono wake na kushika simu yake ya mkononi. Mmmh! Alighuna na kuitolea macho simu yake baada ya kukutana na missed calls tatu kutoka kwa Sekretari wake Esther.

Alitaka kumpigia lakini akasita kidogo kisha akawaza kwa muda “Lakini si sekretari wangu huenda kuna jambo linalohusiana na masuala ya kikazi zaidi” akajaribu kupiga simu lakini kwa bahati mbaya Esther aliyekuwa na kiwewe cha kukosa usingizi kwa kuwaza sana juu ya kumbato zito alilompatia Boss France na kuegemea kifuani mwake kwa muda kidogo kiasi cha kuzidi kumpa uchizi katika fahamu zake.

Kutokana na wenge alilokuwa nalo kwa wakati huo alijikuta akibonyesha sehemu ya kukatia simu badala ya kupokea “Oooh! Mungu wangu, sasa hichi ni nini nimekifanya tena? Alibaki akijiuliza huku Boss France akipata taarifa ya kwamba “Namba unayoipigia inatumika kwa sasa tafadhali jaribu tena badae” Boss  France aliamua kumuandika Vicky ujumbe wa meseji uliosomeka “Hello! Natambua ya kwamba utakuwa umechoka sana lakini pia naomba unisamehe kwa yote yaliyoweza kutokea kwani huikuwa ni dhamira wala kusudio langu hivyo usinichukie wala kunifikiria tofauti, uwe na usiku mwema na ulio tulivu” ujumbe ule ulionyesha kufika lakini hapakuwa na majibu yoyote kutoka kwa Vicky baada ya Boss France kusubiri kwa dakika kadhaa. Aliamua kuitelekeza simu yake na kutojali juu ya kupiga tena simu kwa Esther.

Wakati huo aliikumbuka juice yake ya embe aliyoingia nayo chumbani kisha akaamka pale kitandani mwake na kwenda kuifungua kisha akajipigia pafu kadhaa na kujiegemeza tena kitandani mwake. Punde si punde usingizi mzito ukamzoa, Ilikuwa imekwisha kutimu majira ya saa tatu kamili usiku.

Baada ya Esther kuona kimya kimetawala na hapakuwa na dalili yoyote  ya kupigiwa tena simu na Boss France ilimlazimu amuandikie ujumbe kwa njia ya meseji “Bila shaka utakuwa umechoka na pengine umekwisha kulala lakini nilitaka kukuarifu kwamba kila kitu kiko vizuri ofisini na kama kesho utakuwa vizuri unaweza ukaendesha kikao na mimi nipo kuhakikisha kila kitu kinaenda sawa, nakutakia usiku mwema Boss mwenye jumba lake” Looh..! Ama kweli kila shetani na mbuyu wake. Na waswahili walishasema Unachokisusa wewe cha mnyima usingizi mwenzio... Esther aliusoma mara tatu tatu ule ujumbe wake aliouandika kabla ya kuutuma kwa Boss France kitendo ambacho kilimpotezea si chini ya dakika tano na baada ya kujiridhisha ya kwamba uko sawa aliamua kuutuma.

Hivyo ilimpasa kujipumzisha kulingana na majukumu mazito aliyoweza kuhangaika nayo siku hiyo. Alichukua moja wa mito yake na kuukumbatia kisha akavuta blanketi lake na kuuchapa usingizi. Usiku huo ulikuwa wa aina tofauti kati ya watatu hao hasa kwa Boss France pamoja na Vicky kwani Boss France aliyejihakikishia usingizi wake mapema ya saa tatu za usiku aliweza kushtuka mnamo majira ya saa tisa za usiku kulingana na ndoto iliyomdanganya kwamba alikuwa amelala pamoja na Vicky kitu ambacho hakikuwa na uhalisia wowote. Alishtuka na kujikuta akiita “Vicky... Vicky... Vicky...” akatizama huku na huko hakuweza kuona nyongeza ya mtu yoyote tofauti na yeye jambo ambalo lilikuwa ni gumu kwake kuweza kuliamini.

Alisimama na kutembea kwenye kona zote za chumba chake lakini hakuweza kubaini lolote lile na mwishowe alitikisa kichwa chake na kupikicha macho kwa vidole vyake pengine labda alihisi kama bado hayamtoshi kuona bila ya kufanya hivyo lakini bado ilikuwa ni bilabila. Alisogea mpaka kwenye dirisha kisha akavuta pazia pembeni na kutizama nje aliona jiji likiwa limemeta kwa mataa na baada ya kuyaridhisha macho yake kwa uzuri wa jiji alilazimika kurudi kitandani mwake akavuta shuka na kuendelea kujipongeza kwa usingizi.

Esther naye aliyekuwa amejawa na mawenge ilikuwa ni ngumu sana kwake kwa siku hiyo kupita bila ya kukumbwa na njozi kwani hisia zilizidi uwezo wa fikra zake kwa siku hiyo. Yalikuwa ni majira takribani yaleyale ambapo naye alikitwa na njozi iliyokuwa haielezeki kwa mtazamo wa kawaida. Looh! Jambo lilikuwa jambo kweli. Wakati akiwa katika fikra alisikia mlango wa jikoni ukijibamiza kwa nguvu na kishindo kizito kusikika kisha kukawa kimya kitendo kilichomfanya Esther kuingiwa na wasiwasi pasipo kujua kulikuwa na nini.

MWISHO

ENDELEA KUFUATILIA MIENDELEZO YA TAMTHILIYA HII PENDWA.

Mwandishi: Sebastian Seba

Mawasiliano: 0758162527



Post a Comment

0 Comments