Facebook

PESA ZA SHEMEJI SEHEMU YA 14 (A story by Sebastian Masabha 0758-162-527)




Mbona kama sielewi ina maana sikulifunga gari langu, ila sidhani au nitakuwa nimelewa sana, Mhhh!... hapana.

Boss France alikuwa akimshuhudia rafiki yake akitapatapa kutafuta ufunguo wa gari bila ya mafanikio.

Sasa ina maana unatafuta nini? Funguo wa gari unatafuta kama vile umedondosha akili kwenye katani.. Boss france alizungumza kilevi mno na maneno yake hayakuwa na msaada wowote kusaidia kuupata ufunguo wa gari.

Meneja Tinno alikaa chini kwa mda na kuendelea kufikiri alipoweka funguo wa gari lakini bado fikra zake hazikuweza kufua dafu hata chembe.

Weweee nichukulie poa rafiki yangu lakini mimi ni Standard, Quality, professional yaani niko Comfortably.. lakini embu ngoja kwanza, wewe si nilikukuta pale kaunta na yule muhudumu. Haujaacha kweli pale funguo?

Boss France alizungumza tena, ingawa alikuwa amelewa sana lakini muda huu alizungumza jambo la maana kwa Meneja Tinno.

Ahaaaaah! Kweli hapo umenena sasa. Kwa maneno haya nimeamini kwamba wewe ni Standard, Quality and professional. ama mlewaji mwenye akili...

Meneja Tinno alikubaliana na maneno ya Boss france na kujiaminisha yakuwa lazima funguo wa gari lake utakuwa pale kaunta. Alisogea mpaka pale kaunta na kupaza sauti yake iliyogubikwa na ladha shayiri.

Fetty, Fetty, Fetty... wewe Fetty..

Abeee Boss... Fetty mtakuja aliitika haraka kama vile sumaku ya ngomani ivutavyo mchanga

Meneja Tinno alizidi kuipaza sauti yake kwa ujasiri mkubwa. Haya nipatie funguo zangu nilizoziacha hapa.  Bila ya ubishi Fetty mtakuja alimpatia Meneja tinno funguo hizo huku akimtizama machoni na kuilamba midomo yake.

Eeeh! Wewe mwanamke wewe.., Wallah utakuja kuniuwa bure na vile sina mke hohohooo.. kauli za uropokaji zilizidi uzito fikra za Meneja tinno na kuendelea kumpamba Fetty Mtakuja kwa kubwabwaja sheheni ya Maneno.

Waooh! Kumbe hauna mke jamani na ulivyo pedeshee.. Fetty naye aliona ameanza kupata mlango wa kumwingilia Meneja tinno, huku mawazo yake akiyaelekeza zaidi juu ya pesa za Meneja tinno kwa kuhisi kwamba alikuwa ni mtu mwenye pesa nyingi mjini.

Fetty mtakuja alianza kumteka Meneja tinno kihisia. Na hii ni baada ya kutambua moja ya udhaifu wake uliotokana na kunywa pombe nyingi.

Sasa Boss, hivi unajishughulisha na kazi gani vile? Fetty mtakuja alizidi kumuhoji Meneja tinno, ili azidi kujipatia upenyo zaidi.

Hahahaaa.. hilo ni swali gani la kuuliza mrembo kama wewe, ulipaswa kuuliza jinsi gani utaweza kutumia pesa zangu... Meneja tinno aliendelea kujisahau na kushindwa kufahamu makosa aliyokuwa akiyafanya kwa mhudumu huyo wa kaunta kwa kuendelea kusema.

Kwa vile umeniuliza basi na mimi nitakujibu mrembo Fetty. Ujue mimi nina pesa nyingi, alafu kazi yangu, kazi yangu, kazi yangu... Mmmh!

Mimi nafanya kazi ndani ya Seren..., mara ghafla aliguswa bega na sauti nzito ya kumkemea ikitua katika masikio yake na kumfanya akatishe kile alichokuwa akimwambia Fetty.

Hakuwa mwingine bali alikuwa ni Boss France aliyezinduka kule alipokuwa amekaa na kumsitisha rafiki yake kwa kile alichokiona kilikuwa ni upuuzi, kwa kutaka kuvujisha siri zake kwa mwanamke aliyefahamiana naye kwa mara ya kwanza.

Mazungumzo baina ya wawili hao yalikuwa ya mvutano kidogo huku naye fetty akijaribu kutia lake neno katikati ya wawili hao.

Boss France: Tafadhali naomba tuondoke eneo hili, muda siyo rafiki na tumeshakunywa kupitiliza.

Meneja tinno: Sawa ila nipe dakika kama mia tano hivi kidogo tu niongee na huyu mwanamke.

Boss France: Dakika mia tano looh!. Hivi akili yako ya kawaida inazijua dakika mia tano, ama ni akili za pombe hizi? Hahahaaa..

Fetty Mtakuja: Lakini si umuache mwenzako, azungumze anachojisikia.

Boss FranceWewe, funga domo lako, unamjua huyu ni nani?.. au unazungumza tu sababu mna mdomo.

Meneja tinnoHaya inatosha sasa, wote nimewaelewa, basi tutaondoka.

Boss France: Hapana tena Hapana, Siyo tutaondoka, ndo tuondoke sasa, umesahau kwamba kesho tutatakiwa kwenda wapi na vipi kuhusu maslahi ya kazi yako?

Meneja tinno: Dah! Ila kweli, Kweli kabisa tunapaswa kuondoka eneo hili.

Meneja tinno aliweza kushawishika na maelezo ya Boss France ambayo yalikuwa na tija ya kulinda na kuendeleza heshima ya kazi zao. Aliona hakukuwa na sababu ya kuendelea kubishana na kuvutana kwa ajili tu ya mwanamke ambaye alimfahamu kwa mara ya kwanza bila ya kuuelewa undani wake zaidi.

Boss France alivuta wallet yake na kutoa kiasi cha pesa kulipia gharama zao walizotumia, akamshika rafiki yake mkono kisha wakaondoka.  Fetty mtakuja aliishia kuwatolea macho na kukosa kufanya lolote la ziada, kwani fikra zake na mawazo yake juu ya Meneja tinno kwa usiku huo, ziligonga mwamba.

Walipotoka nje, Boss France aliendelea kugomba sana na kuwa mkali kwa rafiki yake. Ilikuwa ni wazi kwamba hakufurahishwa na kitendo alichotaka kukifanya Meneja tinno.

Boss France: Hivi kumbe ukinywaga pombe kupitiliza, unakuwa kama mweu ndugu yangu.

Meneja TinnoKwanini wasema hivyo.?

Boss France: Unawezaje kutaka kutoa siri zako mbele za watu, au kisa yule mwanamke uliyeweza kuoanana naye kwa siku moja tu?. Alafu pia, hawa wanawake wa baa siyo wa kuwaamini kabisa kwani wengi wao huwa ni machangudoa kupitiliza, wanachokijali wao huwa ni pesa tu kuliko hata afya zao.

Meneja Tinno: Nisamehe bure ndugu yangu, ujue sikuliwaza hilo kabla na pengine ni hizi pombe tu.

Boss France: Angalia pombe zisiwe zinazidi uwezo wako wa kufikiri, mwishowe uje kugeuka kituko na matatizo mbele za watu.

Meneja Tinno: Hili nalo neno kwakweli, lakini mbona wewe mwenyewe ulilewa sana wakati ule mpaka ukaona kama vile Zeyna anapitapita machoni mwako.

Boss France: Ni sawa ila tusianzishe ligi, wewe ni zaidi ya rafiki kwangu hivyo tunaelewesha pale mmoja wetu anapojaribu kukosea lakini pia huwezi jua kama nilikuwa nakuchora kwa wakati ule.

Meneja TinnoSidhani labda unieleweshe vizuri.

Boss France: Sikuwa nimelewa kiasi hicho, alafu ningekuwa mtu wa hivyo nadhani ningeshatembea na wafanyakazi wangu wengi tu.. akiwemo hata huyu aliyefanya tukutane usiku huu.

Meneja Tinno: Sawa nimekuelewa, lakini waweza endesha gari kwa utulivu kweli?

Boss France: Ondoa shaka kuhusu mimi, kwani Mimi ndiye niliyetakiwa kukuuliza swali hilo.

Meneja Tinno: Usijali kabisa mimi nitafika salama ndugu yangu.

Wawili hao waliweza kufikia maridhiano na kila mmoja aliingia katika gari lake na kutimka kuelekea nyumbani kwake.

Boss France: alikanyaga mafuta vilivyo na kufika mapema nyumbani kwake ingawa alikuwa amechoka sana. 

Piiiii piiiii piiiiii honi za gari zilisikika kwa fujo nje ya nyumba. Malila mwanajogini alitoka nje wepesi ili kufungua geti kwani alishabaini honi zile zilikuwa niza gari la Boss wake.

Baada ya geti kufunguliwa Boss France aliingiza gari kwa fujo sana nusura amgeuze nduguye kuwa bamsi la chalinze

Daaah! Boss mbona hivi, wataka kunigeuza chapati mara hii. Alilalamika sana malila na bila shaka aligundua yakuwa Boss wake alikuwa ameshatinga vitu vya London ya buza.

Boss France alishuka huku akipepesuka na kupiga hatua mbili mbele, tatu nyuma na hata asieleweke kama alikuwa akielekea ndani au kutoka nje ya geti. Hakuishia hapo bali aliendelea kubwabwaja maneno yaliyokuwa hayana kikomo. Weeee tulia bwana siwezi kukufanyia lolote baya ndugu yangu

Malila mwanajogini: lakini umenikosakosa hapa ujue

Boss France: Kwani huoni niko fiti ndo maana nimekukosakosa, ningekuwa sielewi-elewi ningeshakugonga hahahaa..

Malila Mwanajogini: Dah! Kwakweli utafika mbinguni umechoka sana..

Boss France: Unasemaje weee.. neno la mwisho umesemaje?

Malila Mwanajogini: Hamna mkuu, nimesema leo umetisha sana Boss kama kawaida yako. Alisogea na kumshika Boss wake kisha akamsindikiza hadi ndani ya chumba chake.

Kwa hali aliyokuwa nayo Boss France haikumruhusu hata kuvua viatu vyake kwani alijiangusha kitandani kama mzigo na kuanza kukoroma. Halikadhalika kwa Meneja tinno alifika nyumbani kwake na kujitupia kitandani moja kwa moja na hata asipate muda wa kumfikiria Fetty mtakuja yule mhudumu wa Baa.

Usiku ulionekana kuwa mrefu lakini kwa Boss France alihisi kama ulitawaliwa na dakika chache za kumfanya yeye kupumzika kwani palikucha haraka pasipo yeye kuumaliza uchovu aliokuwa nao.

Yalikuwa ni majira ya saa mbili kamili asubuhi. Boss France alinyanyua simu na kumpigia rafiki yake Meneja Tinno ili kumjulia hali.

Boss Tinno alipokea simu ya Boss France na kuanza kusikika akipiga mihayo

Aawwagghhh... Asee vipi mkuu?

Boss France: Njema, natumai kumekucha salama ndugu yangu. Vipi kuhusu jana ulifika salama?

Meneja Tinno: Hilo siyo la kuuliza nilifika salama kabisa. Vipi kuhusu wewe?

Boss France: Salama vilevile. Alafu utaondoka na Boti ya muda gani au umechukua ndege Sultan mzee wa kukwea... hahahaa..

Meneja Tinno: Looh! Kweli umenikumbusha jambo la maana, nilikuwa sielewi nawaza nini hasa kumbe leo kuna safari ya muhimu. Kuhusu usafiri Sekretari wangu alifuatilia jana nadhani atanijuza mapema tu.

Boss France: Ooh! Sawa Basi ngoja mimi nikaserebuke na maji mara moja.

Meneja TinnoKhaaa!! Unataka kuangusha chupa tena na hali hiyo mkuu.

Boss France: Hapana haujanielewa, namaanisha naenda kuoga mara moja. Kwa hali hii nikiongeza tena mvinyo nitakuwa mgeni wa nani.

Meneja Tinno: Basi sawa...

Boss France alichukua mswaki na taulo yake na kuelekea bafuni. Aliswaki na kuoga huku akiyafurahia maji. Kwa sauti ya mbali alisikia Sms zikilindima kwenye simu yake.

Alitoka bafuni na kujinyoosha kulia na kushoto kisha akajipangusha maji mwilini mwake. Hazikupita sekunde alisikia Sms nyingine ikiingia kwenye simu yake. Naye bila ya kupoteza muda alianza kuzifungua na kuzisoma moja baada ya nyingine.

Meseji ya kwanza ilikuwa niya sekretari wake Esther. “Hello Boss! habari za asubuhi, natumai umeamka salama. Nitafika hapo kwako muda wa saa nne ili tuondoke pamoja”  Boss France alitingisha kichwa na kujibu ujumbe ule kwamba “Sawa, karibu sana”

Kisha akaendelea kusoma meseji nyingine. Na hii ya pili ilikuwa niya Meneja Tinno “Mkuu nimepata ujumbe kutoka kwa sekretari wangu kwamba tutaondoka na Azam Marine ya saa sita bila shaka nawewe jana ulinijuza kitu kama hicho”

Boss France alilazimika kujibu ujumbe kutoka kwa meneja Tinno. “Ooh! Vizuri basi tutakuwa pamoja Boss”

Meseji zilikuwa nyingi lakini baada ya kupitisha macho yake kwa haraka haraka akagundua yakuwa tayari amekwisha malizana na zile za muhimu. Boss France aliendelea na maandalizi yake ya safari kwa kuanza kupanga nguo na vitu vingine vya muhimu alivyoona vitamfana huko aendapo.

Lakini ghafla akakumbuka yakuwa Esther alimtaarifu yakwamba atampitia nyumbani kwake ili waondoke kwa pamoja. Boss france alipaza sauti yake kumtaka Malila mwanajogini afike mara moja kupokea maelekezo.

Naam Boss malila mwanajogini aliwasili mapema kama alivyohitajika

Boss France: Kuna mgeni atakuja mda si mrefu sasa.. ahahaa...

Malila mwanajoginikwani vipi Boss, ni nani huyo?

Boss France: Ni yule sekretari wangu

Malila mwanajoginiahaah! Esther siyo, ama mwingine Boss?

Boss France: Ndiye, kwani umemjuaje? Boss france alifanya mazungumzo yawe ya swali juu ya swali.

Malila Mwanajogini: Hahahaa Boss mbona huwa unamzungumziaga mara nyingi pamoja na yule nani... sijui...

Boss France: Nani huyo tena?

Malila mwanajogini: Yule mwingine.. aaahh .. ngoja nimkumbuke kidogo. Malila mwanajogini alifikiri kwa sekunde kadhaa na kuendelea na mazungumzo baada ya kupata majibu kamili. Anaitwa Vicky kama sijakosea

Boss France: Hahahaa Vicky... hahahaa embu tuyaache haya.  Sasa embu andaa chochote kwa ajili ya Esther

Malila mwanajogini: Vipi kuhusu wewe

Boss France: Usijali kuhusu mimi, unaweza ukaendelea

Malila mwanajogini: Sawa Boss.

Wakati Boss France akiendelea na zoezi lake la kupanga vitu. Mawazo yalimjia juu ya safari yao itakavyokuwa papo hapo akasitisha jukumu lake la kuendelea kupanga vitu.

“Nadhani itakuwa safari nzuri sana japo niya masaa machache, bila shaka nitaenjoyi sana na wenzangu kwani sijawahi safiri kwa usafiri wa kutumia chombo cha maji, Azam marine hiyo kama naiona vile alafu mara ndo paap pembeni amekaa Zeyna hahahaaa...” Boss France alijiwazia huku mawazo yake yakienda mbali zaidi ya fikra zake. Hakika ilikuwa ni moja ya safari iliyotaka kumpa kiwewe licha ya yeye kusafiri mara nyingi hadi kwenye nchi za ughaibuni kuiwakilisha kampuni yake.

Boss France alitaka kuendelea na mawazo yake ya kusadikika lakini mara ghafla alishtushwa kusikia sauti ya Esther aliyekuwa akikaribishwa Sebuleni na malila mwanajogini.

Eheeh! Huyo ni Esther ashafika, yuko moto kweli kwani ratiba zake huwa anazipangilia vilivyo

Boss, Boss mgeni wako ashafika huku alikuwa ni malila mwanajogini akitoa taarifa yenye harufu nzuri iliyokwisha kumfikia Boss France mapema sana.

Nakuja, nakuja namalizia jambo kidogo hapa. Boss france alijibu huku akitizama saa yake na kugundua yakuwa muda ulikuwa siyo rafiki sana. Alimaliza kupanga vitu na kuvaalia kwa uharaka suti nyeusi iliyomkaa vilivyo huku akiyatikisa kidogo mabega yake. Mahojiano ya kupendeza kwake yalikuwa ni kati yake na kioo chake cha ukutani. Alijitazama na kujipa maksi zilizouridhisha moyo wake.

Alitoka ndani ya chumba chake baada ya kujipalilia na marashi yaliyokuwa na manukato ya kunukia kiasi cha kuwavutia njiwa kuja kizipiga filimbi.

Boss france alitembea kwa madaha kuelekea alipokuwa amekaa Esther ambaye alishindwa kujizuia kuonyesha tabasamu lake na kushindwa hata kuficha furaha yake aliyokuwa nayo siku hiyo kwani alisimama na kumkumbatia Boss wake.

Woow.. Boss umependeza sana...

Naye Boss france alicheka kidogo na kuonyesha tabasamu la aina yake kisha akasikika akisema “Asante sana Esther, nawe umependeza vilivyo kama ilivyo kawaida yako”

Wakati hayo yakiendelea Malila mwanajogini alibakia kuwa kushuda na kushindwa kujua ni wapi angelielekeza tabasamu lake kati ya wawili hao zaidi ya kubakia kujichekesha.

MWISHO

ENDELEA KUFUATILIA SEHEMU ZIJAZO ZA TAMTHILIYA HII. BILA YA KUSAHAU KUFUATILIA ORODHA ZA TAMTHILIYA ZA MTUNZI NA MWANDISHI SEBASTIAN S. MASABHA.

1.   PENZI LA MASHAKA

2.   SUKARI YA KIJIJI

3.   KONEKNESHI ZA VALENTINE

Na shairi la

DIMBA LA MKAPA 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

Post a Comment

0 Comments