
SEHEMU YA KWANZA 01.
Ilikuwa
yapata majira ya saa moja kasoro jioni, Ambapo ilisikika sauti mithili ya mtu
aliyekuwa akitafakari na kujihoji mwenyewe juu ya jambo fulani huku akisema “Zey..zey..!
Aah! Kumbe ndo binti yule mrembo ama kweli wapo walioumbwa wakaumbika” Sauti
hiyo ilikuwa ikitaja jina la msichana aliyeonekana kuwa mrembo sana pasipo
kulimalizia kiasi cha kufananishwa na mtu mwenye ukakasi katika ulimi wake na
mwenye kigugumizi kikali. Huyu alikuwa ni France Meneja mkuu wa moja ya Five
star hotel “HYATT REGENCY. The Kilimanjaro Hotel” ya Jijini Dar-es salaam. Pia
alikuwa ni kijana mcheshi wa makamo hivi, mtanashati sana na aliyeishi maisha
ya kifahari. Kwani mbali na kuwa na nafasi ya umeneje mkuu pale Hyatt Regency.
Alikuwa na miradi mbalimbali na mmiliki wa nyumba tatu kubwa ikiwemo moja ya
ghorofa ambayo ndiyo aliyokuwa akiishi ndani ya eneo la Oyster bay. Sambamba na
hilo ua wa nyumba yake ulipambwa na magari ya kifahari kama vile Range Rover,
Land cruiser Vx V8 na Toyota Harrier New model. Kwa ufupi alikuwa ni mtu
aliyejikamilisha kwa kina na aliyeishi maisha ambayo vijana wengi wa kisasa
wangetamani kuyaishi. Basi kutokana na uchovu wa majukumu ya kiofisi aliyokuwa
akiyatekeleza kila siku, yalimfanya ajitupe kitandani na baada ya mda mfupi
alichukuliwa na usingizi mzito uliomfanya aote ndoto sukari usiku wa manane
kiasi kwamba alihamishwa katika dunia nyingine. Hatimaye palipambazuka na
aliamshwa kutoka kwenye wimbi kubwa la usingizini na mwanga wa jua uliokuwa
ukimulika upande wa dirisha lake. “Ahaah! Kumbe kumekwisha kucha” alijisemea
France. Alichukua mswaki wake akaweka dawa kisha akautia kinywani mwake na
kufunga taulo lake akaelekea bafuni. Wakati akiendelea kuswaki kunako sinki
alielekeza macho yake yalioonekana kuwa na dalili za ugairi katika kioo kilichokuwa
sehemu ya juu ya sinki. Na hali hii ilitokana na mwanga wa taa uliokuwa
ukionekana katika kioo hicho. Baada ya kumaliza kuswaki alifungua taulo na
kuliweka kando kisha akaitanguliza miguu ndani ya bafu lake la kukaa (sitting
bathroom) lililokuwa na mng’ao wa kupendeza wa rangi ya dhahabu. Alifungua koki
zote mbili zilizokuwa zikitolea maji moto na maji yenye ubaridi na kuanza
kusafisha sehemu zake za mwili. Wakati akiendelea na zoezi hilo ghafla zilimvaa
kumbukumbu na taswira za yule mwanamke aliyekuwa akimtaja kwa kigugumizi “Zey,
Zey” mapema ya usiku wa jana. Lakini alitikisa kichwa kulia na kushoto
kuashiria kutokubaliana na hali ile. Mara akakurumuka katika maji mithili ya
mbwa aliyechomoka salama katikati ya kundi la wahehe. Looh! Jambo lile lilionyesha
ishara yakuwa France alishanza kuzidiwa na uzito wa mawazo ya mara kwa mara juu
ya mtu fulani aliyehisi kuanza kuzama kwake taratibu kihisia na kumpenda. Baada
ya kutoka bafuni aliingia ndani ya chumba chake kilichokuwa na mahadhi ya
kifalme na kuanza kuvaa nguo kwa ajili ya kuelekea kazini. Siku hiyo alivalia
suti yake ya rangi ya Dark blue
iliyonyongewa na tai ya rangi nyeusi yenye vidotidoti vyeupe na chini
aligongelea moka ya rangi ya maroon iliyowakaka kama ngozi ya chatu. Looh!
Mitupio na mikato hiyo ya kipapaa ndiyo moja ya sababu ya vitu vilivyompa
heshima kubwa na kupendwa na watu wengi wakiwemo wafanyakazi wenzake. Punde
baada ya zoezi hilo France alipulizia perfume ya Mirace katika pande zake mbili
za kwapa na hapo akawa na imani ya kujiridhisha kwamba yuko tayari kwa ajili ya
kuelekea ofisini. Kuja kutizama katika saa yake ilikuwa imekwisha kutimia
majira ya saa mbili 8:00 am asubuhi akashtuka kidogo na kujisemea Aghaa! “Kumbe
muda umeshasogea kiasi chake hivi acha niwahi kwenye kula yangu” kisha
akaachia tabasamu lake lenye uwezo wa kumshibisha mwanamke yoyote mwenye njaa
kali ya kutokuwa na furaha. Alielekea nje kutoka ndani ya mjengo wake wa
thamani na kuyatupia macho moja kwa moja katika gari zake kisha baada ya
sekunde chache akawa amekwisha kupata majibu ya kwamba na gari lipi lingemfaha
zaidi katika shughuli zake za siku hiyo. Alichagua gari lake la land cruiser Vx
V8 na ambalo alionekana kulipenda zaidi maana ndilo alilokuwa akilitumia mara
kwa mara. Akapanda ndani ya chuma cha Mjapani na kisha safari ya kuelekea
kazini kwake ikaanza. Wakati akiwa njiani alikuwa akiyashibisha masikio yake
kwa ladha tamu ya mziki asali wenye mahadhi ya kimambele. Ilimchukua takribani
muda wa nusu saa hivi kuwasili katika eneo lake la kazi na hapo ilikwishakutimia
majira ya saa mbili na dakika thelathini na tano 8:35 am asubuhi. Mara tu baada
ya kushuka katika gari lake akapokelewa na sauti iliyosikika “Hello! Boss
France” Akaitikia “Hello” kisha kimya cha muda kidogo kikatawala baina ya
wawili hao. Sauti hiyo ilikuwa ni nyororo sana na tamu zaidi katika masikio ya
Boss France kiasi cha kwamba ingeweza kutumika kama Bank Card ya kuchomolea
rundo la pesa katika mashine ya ATM. Bila shaka sauti hiyo ilikuwa niya mmoja
wa wafanyakazi wenzake katika Hotel hiyo ya Hyatt Regency na aliyetambulika kwa
jina la Vicky. Vicky alikuwa ndiye mhasibu mkuu katika Hotel hiyo na pia
alikuwa na msichana mrembo na mcheshi wa aina yake. Baada ya salamu ile Boss
France alianza kupiga hatua kwa mwendo wa madaha na kuelekea ndani ya lift
iliyompeleka moja kwa moja karibu na ofisi yake. Alifungua mlango na kuingia
ndani ya ofisi kisha akavua koti lake la suti na kuwasha Air condition A/C
iliyotoa upepo wenye ubaridi mwanana. Aliketi katika kiti chake cha kuzunguka
na kujizungusha mizungusho miwili huku akigonganisha vidole vyake viwili na
kutikisa kichwa chake upande wa kulia na kushoto. Baada ya kufanya zoezi hilo
kwa muda mchache Ghafla simu yake ya mkononi ikaita naye alisita kuipokea na
mara baada ya kukata ikaita kwa mara ya pili na Boss Fance akajisemea “Huyu
atakuwa ni Fausta mpenda mizinga” lakini baada ya kuitoa aliona namba ngeni na
kuipokea Looh! Boss France alizizima ghafla na kuganda kwa mshangao ulioonekana
katika uso wake mithili ya mtu aliyepigwa na butwaa zito, kwani sauti ile
ilikuwa ikifanana na sauti ya mrembo aliyehisi kuanza kumtawala katika mawazo
yake. La hasha! Sauti hiyo ilikuwa tamu zaidi na yenye ladha ya aina yake kwani
ilipenya mpaka kwenye mishipa ya visigino vya Boss France. Ilikuwa ikisema
Hello! Big Boss naomba leo tuonane kwa ajili ya maongezi muhimu sana kama
hautojali kisha simu ikakata ghafla. Wakati huo Boss france alikwisha shikwa na
kimuhemuhe cha kutaka kujua ile ilikuwa ni sauti ya nani na wangekutana wapi na
kwa muda gani lakini ikashindikana kwa muda huo kwani aliponyanyua simu yake na
kuipigia namba ile alipokelewa na majibu ya wahudumu wa voda “Namba unayoipigia
haipatikani kwa sasa tafadhali jaribu tena baadae”...............................
Mwisho wa
sehemu ya kwanza.
Je nini
kitakachoendelea baada ya Boss France kubahatika kuipigia namba ile na
kupokelewa na mhusika?
Endelea kufuatilia mwendelezo wa tamthiliya hii katika sehemu ya pili
Mwandishi: Sebastian Masaba.
0 Comments