Facebook

SUKARI YA KIJIJI (SEHEMU YA KWANZA)



Ilikuwa ni jioni majira ambayo jua lilionekana kuelekea kuchwea,  upepo nao ulivuma kwa kasi huku ngurumo za radi nazo zikisikika kwa mpasua mkubwa. Kiza totoro kilianza kutanda na mwanga wa radi uliosambaa na kumulika uligubika katika kijiji cha Korona. Matone membamba na mepesi yaliyofuata mwelekeo wa upepo mkali nayo yalianza kushuka ndani ya Kijiji cha Korona.

Siku hiyo ilikuwa ni siku ya tofauti ndani ya kijiji cha korona kwani hapakusikika mtu wala kitu chochote tofauti na ngurumo za radi zilizokuwa zikipasua mibuyu na mpingo hapo Kijijini. Baada ya muda kidogo mvua ilizidi kuongezeka na kunyesha kwa kiasi kikubwa hali ambayo ilipelekea kujaa kwa mto Yambwa,  mto uliokuwa mkubwa na maarufu sana hapo kijijini.

Ndani ya nyumba ya mzee Magoti ukimya ulitawala kwa kiasi cha kukidhia, Familia ya mzee magoti ilikuwa ni familia ya wake wawili pamoja watoto tisa. Ilikuwa ni moja ya familia maarufu sana na iliyoheshimika kwa upekee wake ndani ya kijiji cha korona. Mzee magoti alikuwa ni mzee Mcheshi na mchangamfu kwa kila mtu hapo kijijini na umaarufu wake ulitokana na busara,  hekima na uwezo wake mkubwa wa kumiliki mali nyingi na zenye thamani hapo Kijijini. kwani alikuwa akimiliki Ng'ombe wengi si chini ya Elfu tatu pamoja na Mashine za kusagia mahindi, mtama na mashine ya kukuboa ngano na mpunga.

Umaarufu na sifa kidekede alizokuwa nazo Mzee Magoti hazikuishia hapo kwani alikuwa ni Mzee ambaye pia alimiliki mashamba makubwa ya mikonge, karanga, mahindi miwa na michungwa yaliyokuwa yakizidi kumuweka karibu na watu wengi hasa wasiojiweza hapo kijijini. Katika kijiji cha korona palikuwa na tatizo moja kubwa la uvamizi na uwizi wa mali kama vile mifugo na mazao lililokuwa likifanyika na watu wa vijiji vya jirani suala ambalo lilichangia kuleta maafa mengi na kuwarudisha nyuma kimaendeleo watu wengi sana hapo kijijini.

Lakini ilikuwa ni ngumu sana kwa mzee Magoti kukubwa na hujuma hizo kwani alikuwa na ulinzi mkali na mkubwa wa mbwa wengi pamoja na ulinzi wa kijadi. Hali ya ngurumo na mwanga wa radi iliyochanganya na mvua kubwa bado iliendelea kufanya ukimya kwa watu wengi hapo kijijini. Ghafla! kwa mbali zilisikika kelele za watu waliokuwa wakiashiria kuomba msaada. Alikuwa ni Kijana zahera mtoto mdogo nawa mwisho wa Zuena mke wa kwanza wa Mzee magoti aliyeweza kuwa wa kwanza kusikia sauti hizo kwa wakati huo.

Sauti hizo zilimshtua sana na kumfanya azidi kuogopa kwani mapigo yake ya moyo yalimwenda mbio sana na kumfanya azidi kukumbatia shuka. Sauti hizo ziliendelea kusikika tena kiasi kwamba hata naye mijanja mtoto mkubwa wa zuena alikuwa akizisikia kwa mbali. Zahera alishindwa kuendendelea kuvumilia akakurupuka na kukimbilia katika chumba walichokuwa wakilala wazazi wake “ngo, ngo, ngo.  ngo,  ngo, ngo.” Aligonga mlango kwa nguvu huku akihema kwa uwoga “nani wewe?” mzee  magoti mwenye kibezi kizito cha kumtoa chura matopeni aliuliza  Baba,  baba ni mimi zahera kuna shida huku” na papo hapo mzee Magoti alishtuka sana na kutoka nje akiwa na panga mkononi huku taulo lake jeupe likiwa kiunoni. Alijitia ujasiri huku akionekana kuwa na kimuhemuhe cha kutaka kujua ni nini kilichotokea.

Wakati huo mzee Magoti alimuona mwanaye akiwa katika hali ya uoga sana na kabla hajaendelea kuhoji juu ya jambo lolote,  ghafla mwanga mkali mweupe ulimulika na uliofuatiwa na ngurumo kubwa ya radi na kumfanya mzee Magoti ajikute yumo chini ya uvungu wa kitanda chake bila ya kujali alimuacha wapi mwanaye Zahera kwa wakati huo. Alijimudu ndani ya sekunde chache na kutoka chini ya uvungu haraka haraka kisha akaelekea tena nje ya chumba chake na mara hii alikuwa amebeba panga pamoja na rungu kubwa. Zuena ambaye ni mke mkubwa wa mzee Magoti naye alishtuka kutoka katika usingizi mzito ingawa tukio lile lilikuwa limeshampita na usiweze kufahamu juu ya chochote kilichotokea kwa wakati huo.

Mzee Magoti naye alielekea katika chumba alalacho mwanaye Zahera huku akitoa sauti ya chini chini tena iliyogubikwa na uoga kwa kuita “Zahera,  zahera,  mwanagu huko wap..?” “Niko huku Baba” Wakati Zahera akiyasema hayo kwa Baba yake mara ghafla zikasikika tena zile sauti zilizikuwa zikiashiria kuomba msaada kwa mara ya tatu. Mzee Magoti hukuwa na budi kuanza kunyata taratibu huku akielekeza nyayo zake kwenye chumba cha mwanae mkubwa Mijanja. Mijanja alikuwa ni kijana jasiri na shupavu ambaye mara kadhaa alikuwa akifanya matukio ya kishujaa yaliyowaacha vinywa wazi wanakijiji wa kijiji cha Korona kwani umahiri wake na ujuzi wake wa kutumia mkuki, pinde za mishale pamoja na kucheza na panga ulimpa umaarufu na kuzidi kuifanya familia ya Mzee Magoti kuwa almasi ndani ya kijiji cha Korona.

“Ngo, ngo, ngo Mijanja... Mijanja” mzee Magoti aliugonga mlango wa chumba cha kijana wake kwa nguvu huku akiita mara mbilimbili kwa lengo la kutaka kupata msaada wa haraka. “Naam Baba kuna jambo gani tena usiku huu mbona kijeshi namna hii” aliuliza mijanja ambaye naye hakuonyesha kama alikuwa katika hali ya usingizi. “Kuna kelele za watu zimesikika upande wa mto yambwa zikihitaji msaada” alijibu haraka haraka mzee Magoti. “Ahaah! Hata mimi pia nimebahatika kuzisikia na tena si mara moja ijapokuwa sikupata jibu la nini chakufanya” alisema Mijanja ambaye alikuwa akifungua mlango wa chumba chake huku akiwa amebeba Kurunzi yenye mwanga mkali, upinde mgongoni pamoja na podo iliyotiliwa mishale kadhaa. Walifanya himahima kuanza kuelekea katika eneo la mto yambwa na hapo Mzee Magoti hakuweza kuwa na wasi kwani kiburi cha tambo na ujasiri kilimjaa kutokana na uwepo wa mwanae mwenye hadhi ya tuzo manuwari za kishujaa.

Wakati wakielekea katika mto yambwa Mtoto Zahera naye aliyeamriwa kubaki nyumbani alikuwa akiwafuatilia kwa nyuma licha ya kujali udogo wake pamoja na giza nene lililokuwa limetanda siku hiyo. Ilikuwa ni ngumu kwa Mzee Magoti pamoja na mwanaye mijanja kuweza kutambua yakwamba kijana Zahera alikuwa akiambatana nao kisirisiri. Njiani palikuwa kimya sana, kwani ulikuwa ni mwendo wa mguu na njia,  baridi nayo ilikolea katika miili yao kiasi cha kufanya hata mikono yao kuhisi ganzi nayo makundi ya bundi waliokuwa wametanda katika miti mbalimbali walikuwa wakiimba ukuti ukuti kwa ngurumo zao. Walipoukaribia mto yambwa kwa mbele kidogo walibahatika kuona mwanga wa tochi uliokuwa ukiangaza huku na kule, ikiwa ni ishara tosha yakwambwa palikuwa na kundi la watu wachache waliokuwa wakiangazia juu ya jambo fulani. Mzee Magoti na mwanaye Mijanja walijibanza pembezoni mwa mti mrefu naye mijanja aliokota kipande cha jiwe na kukirusha kuelekea kwenye lile kundi la watu. Ebooh! Kundi lile lililokuwa na watu watatu walioshindwa kujulikana walikimbilia na kutokomea upande mwingine wa mto yambwa.

Waliendelea kusogea kwa ukaribu zaidi na mto yambwa wakazunguka huku na kule wakati huo Mijanja aliliwasha kurunzi lake lililokuwa likiachia mwanga mkali uliokuwa na uwezo na kummulika mnyama jamii ya simba na kumfanya azimie kwa muda kutokana na ukali na wanga huo. Mara ghafla Zahera aliyekuwa akiwafuatilia kwa nyuma alipiga kelele yenye mshtuko iliyoweza kuwashtua na kutaka kumfanya Mzee Magoti atoke mafuta kukimbilia mtoni.

Mijanja aligeuka kwa ujasiri na kutaka kuanza kufoka kwa hasira kwa uwepo wa Zahera katika tukio lile hatarishi. Lakini kabla ya kutaka kufanya hivyo alimuona mtu aliyekuwa amelala chini huku akionyesha kuwa na hali mbaya ya kuzidiwa. “Baba Baba kuna mtu hapa” aliongea Mijanja huku akipiga magoti yake chini na kuanza kuanza kutoa msaada wa haraka haraka kwa mtu yule. Alipomchunguza vizuri aligundua yakuwa mtu yule alikuwa niwa jinsia ya kike. Looh! Mapigo ya moyo yalimwenda mbio mijanja kwa kuhisi huruma juu ya yule msichana na asiwezejua ni kipi kilichokuwa kimemkuta. Kulingana na hali aliyokuwa nayo msichana huyo Minjanja hakuwa na budi kumsaidia kwa namna yoyote ili kuhakikisha anafanikiwa kuinusuru roho yake. Aliupeleka mkono wake wa kulia na kuanza kumpapasa yule msichana. na kwambali aliweza kuyasikia mapigo ya moyo ya yule msichana yakidundadunda. Looh! Aligundua yakuwa alikuwa bado ni mzima. Mijanja alimsogelea msichana yule kwa ukaribu zaidi na kuelekeza midomo yake katika pua na kuanza kuvuta na kumpulizia pumzi kwa haraka haraka huku akiyasikilizia mapigo ya moyo ya msichana huyo aliyeonyesha kupigwa na maji mengi yaliyomzidi uwezo.

Mijanja aliendelea kufanya hivyo kwa muda na mara hii alimvika msichana yule koti alilokuwa amelivaa na  kumkubatia kwa kumganda kama ruba ili aweze kumpatia joto katika mwili wake.

 Ilichukua mda kidogo kwa msichana huyo ambaye hawakuweza kumfahamu kuanza kukohoa kama mtu aliyepaliwa na maji yaliyoingia katika koo la hewa. Mijanja alitazamana na Baba yake Mzee Magoti huku kila mmoja akiachilia tabasamu lililoonyesha dalili za ushindi juu ya tukio lile. Nazo radi zilizokuwa zikitoa mwanga mkali ziliendelea kunguruma kwa sauti kubwa na kukituliza tuli kijiji cha Korona. Mijanjaa alimnyanyua yule msichana na kumweka juu ya bega lake kisha wakaanza safari ya kuelekea nyumbani kwa Mzee Magoti.

Safari hiyo ilionekana kuwa ndefu kutokana na baridi iliyokuwa ikizidi kupuliza. Mzee Magoti hakutaka kukaa mbele wala nyuma na hii ni kutokana na tabia yake ya uoga uliopitiliza kiasi cha kwamba alizidiwa mbinu na mwanaye Zahera aliyeonekana kuwa shupavu licha ya udogo wake.

Hatimaye baada ya safari kuwa ni hatua walifika ndani ya boma la mzee Magoti huku wakiwa wametepeta kwa baridi kali. Mijanjaa alimuingiza msichana yule katika moja ya chumba kilichokuwa hakitumiki kisha akamlaza kitandani na kumfunika kwa blangeti zito. Mwili wa msichana yule ulikuwa ukitetemeka sana mithili ya genereta lililokuwa limepungukiwa mafuta. Mijanja alionekana kuwa mwingi wa huruma na mwenye huzuni kila alipokuwa akimtazama msichana yule hata naye Zahera kijana mdogo jasiri alikuwa mwenye kujawa na uso wa huzuni.

Wakati huo mzee Magoti aliyekuwa ni mwingi wa uchovu alielekea kulala katika chumba chake, Mtoto zahera alijilaza pembeni ya msichana yule na kupitiwa na usingizi mzito. Mijanja naye alionyesha kuchoka na kuhisi maumivu mabegani mwake kutokana kazi kubwa aliyoifanya ya kumbeba yule msichana kutokea mto yambwa. Baada ya kitambo kidogo alijisogeza karibu na msichana yule kisha akambusu katika paji lake la uso na kuelekea chumbani kwake kulala. Majira yalikwenda na kujongea sana,  Jogoo nao walisikika wakianza kufokea kijiji cha Korona nazo dalili za mawio zilianza kushamiri. Alikuwa ni Mijanja aliyekuwa wa kwanza kushtuka kutoka katika usingizi na hapo hapo akili yake iliwazia juu ya yule msichana. Akatoka ndani ya chumba chake na kuelekea katika chumba alichomlaza yule msichana. Loooh! Mijanja alibaki kutoa macho kwa mshangao mkubwa kwani aliambulia tu kumuona mdogo wake Zahera pale kitandani akiwa amejifunika blangeti na yule msichana hakuwamo ndani ya chumba hicho. Alitoka nje ya chumba kile huku akiita kwa nguvu “mgeni,  mgeni wewe binti mgeni” na wala hapakuweza kuwa na jibu lolote. Aliweka mikono yake miwili kichwani na kurejea katika chumba chake huku mochozi ya uchungu yakimtoka.

***MWISHO***

 

ITAENDELEA,  USIKOSE MIENDELEZO YA TAMTHILIYA HII KILA SIKU YA JUMAMOSI.

 

A story by Sebastian Masabha:0758162527

 

Post a Comment

2 Comments